Sunday, July 19, 2015

MAMBO 7 MUHIMU KUFANYA ILI UWE NA AFYA BORA MWAKA HUU

Leo ni mwaka mpya.Hongera kwa kumaliza mwaka 2010 salama.MiNi wakati wa maazimio mapya. Miongoni mwa maazimio(resolutions) zinazoongoza ni pamoja na ile ya kuishi maisha yaliyo na afya bora zaidi na furaha. Afya na furaha ni mambo mawili makubwa sana katika maisha yetu.Ukichunguza sana takribani kila kitu tunachokifanya ni katika mpambano wa kimaisha wa kuwa na afya bora zaidi na kuwa na furaha.
Baada ya msimu wa sikukuu ambao hujaa kula,kunywa nk watu wengi huazimia kwanza kupunguza uzito ambao mara nyingi huwa umeongezeka maradufu kutokana na kula na kunywa kwa wingi wakati wa sikukuu.Inaeleweka.Sio utamaduni wetu kwenda kwa mtu kisha ukakataa kula. Katika jamii nyingi hususani zetu za kiafrika,kufanya hivyo ni kosa!Ukizungukia nyumba 10 kwa siku ni bora ujiandae kula au kunywa katika nyumba zote 10. Matokeo yake huwa ni kuwa na kilo za ziada kidogo pindi msimu unapokwisha.
Lakini utafanya,unatakiwa au unawezaje kuwa na afya bora kwa mwaka mzima na sio mwezi mmoja tu wa January baada ya kula na kusaza wakati wa msimu wa sikukuu?Hilo ni swali ambalo thamani yake ni zaidi ya dola milioni moja…a million dollar question. Sote tunakubaliana kwamba afya bora ndio kila kitu.Ukiwa tajiri kupindukia halafu ukawa na afya mgogoro,ni wazi kwamba huwezi kuzifurahia hizo hela zako.
Yafuatayo ni baadhi ya mambo unayoweza kuyafanya ili kuwa na afya bora katika mwaka huu wa 2011.Lakini kabla sijaendelea mbele sana,naomba niweke wazi kwamba afya bora haihusu kula vizuri na mazoezi peke yake bali pia fikra chanya(positive attitude). Kuna umuhimu wa kuhakikisha kwamba siku zote unakuwa na mawazo chanya na pia kuwa karibu zaidi na watu wenye mawazo chanya.
  1. Kunywa Maji kwa wingi- Bila shaka unakumbuka msemo “Maji ni Uhai”.Hiyo ni kweli kabisa.Maji ni uhai sio tu kwa mazingira yetu na dunia kwa ujumla bali pia kwa afya au miili yetu.Maji ni kitu muhimu sana kwa afya zetu.Asilimia 60% ya miili yetu imetengenezwa au imesheheni maji. Maji yanahitajika kwa ajili ya kuondoa takataka au vitu visivyofaa kutoka mwilini.Maji ndio hubeba virutubisho na oxygen.
    Kiasi cha maji anachohitaji mtu kinategemea na mambo kadhaa kama vile unyevu(humidity) wa mahali ulipo,shughuli zinazohusisha mwili anazozifanya mtu na pia uzito wa mwili.Pamoja na hayo,kwa wastani miili yetu inahitaji lita 2 na nusu mpaka 3 za maji.Vyakula tunavyokula huchangia kama asimilia 20% za maji katika miili yetu.Kwa hiyo tunahitaji kunywa maji kiasi cha lita 2 mpaka lita 2.4 au glasi 8-9 za maji kwa siku.
    Njia rahisi ya kujua kama mwili wako una maji ya kutosha ni katika kuangalia mkojo. Mkojo wako unatakiwa kutokuwa na rangi(colorless) au kuwa wa njano kidoogo.Kinyume cha hapo ni ishara kwamba hauna maji ya kutosha mwilini.Njia nyingine kutambua ni pamoja na kukaukwa na midomo(lips) na hata ulimi na pia kupata kiasi kiduchu cha mkojo.
  1. Pata Usingizi wa Kutosha: Unakumbuka tulipokuwa wadogo wazazi wetu walisisitiza sana kwamba twende tukalale mapema ili tukue? Bila shaka walikuwa wanajua kwamba usingizi ni sehemu muhimu sana katika afya. Ukiachilia mbali faida za usingizi kwa ajili ya afya za akili/ubongo wetu,usingizi au mapumziko ya kutosha ni muhimu kwa miili.Afya njema huenda sambamba na mapumziko.Ni wakati wa kuupa mwili nafasi ya kujijenga,kujiongezea nguvu na muhimu zaidi kuhakikisha kwamba tunakuwa na akili timamu. Pia ukosefu wa usingizi ni chanzo cha kuzeeka mapema.
  1. Fanya Mazoezi- Hili linaweza kupita bila maelezo ya ziada.Mazoezi ni muhimu sana kwa afya bora. Fanya mazoezi angalau mara tatu katika wiki.Jipatie muda wa kutembea japo kwa dakika 30. Kama inawezekana nenda Gym.Badala ya kupanda lifti pale kazini kwako au mitaani,tumia ngazi za kawaida.Egesha gari lako mbali kidogo na unapokwenda ili upate nafasi ya kutembea nk. Muhimu zaidi ni kuchagua aina ya mazoezi unayoipendelea. Mazoezi hayatakiwi kuwa adhabu.
    Faida za mazoezi ni pamoja na kujiepusha na magonjwa mbalimbali,kupunguza unene(bila shaka unajua kwamba unene kupindukia sio afya bali ni ugonjwa na sababu kubwa ya maradhi mengine)
  1. Kula Matunda Kwa Wingi-Matunda ni chanzo kizuri sana cha madini na vitamins ambazo miili yetu inahitaji sana kwa ajili ya afya bora. Unajua kwamba machungwa,kwa mfano, yana faida kubwa zaidi kiafya kuliko vidonge vya Vitamin C unavyobugia kila leo? Aina mbalimbali za matunda ambayo yana virutubishi vingi zaidi kiafya ni Parachichi(Avocado),apple,matikiti maji(cantaloupe),Zabibu(Grapefruit),Kiwi,Guava,mapapai,machungwa, strawberries nk.
  1. Kula mboga za majani- Kama ilivyo kwa matunda,mboga za majani(vegetables) ni muhimu sana kwa afya zetu. Wataalamu wa afya wanashauri kwamba tule aina 5 mpaka 9 za mboga za majani na matunda.Jitahidi kupata angalau zaidi ya aina 5 za mboga za majani na matunda.
  1. Punguza Kula Vyakula vya Makopo- Kutokana na jinsi dunia inavyozidi kwenda mbio,watu wengi huwa tunakosa muda wa kupika.Matokeo yake tunakimbilia kwenye vyakula vya kwenye makopo ambavyo ndivyo vimejaa katika maduka na ma-supermarket. Jitahidi kuviepuka vyakula hivyo kwa kadri unavyoweza.Mara nyingi vyakula vya makopo huwa na ingredients ambazo hazifai kwa afya zetu.Kwa mfano,vingi miongoni mwa vyakula hivyo huwa na chumvi nyingi kitu ambacho ni chanzo cha High Blood Pressure na maradhi ya moyo. Unaposhindwa kabisa kujizuia kununua vyakula hivyo vya makopo jaribu kuangalia ambavyo havina sukari au chumvi.
  1. Jipende- Kama nilivyodokeza hapo mwanzo,afya bora huenda sambamba na afya ya akili/ubongo.Njia mojawapo ya kupata afya hiyo ni pamoja na kujipenda.Pengine unajiuliza,kuna mtu ambaye hajipendi? Ukweli ni kwamba pengine ni kweli kwamba hakuna mtu ambaye hajipendi.Tofauti inakuja pale mtu anapofanya vitu ambavyo ni kinyume kabisa na mapenzi ya mwili.
    Mfano,uvutaji sigara,unywaji pombe kupindukia,kutojisafisha mwili wako kwa mfano kuoga,kupiga mswaki na pia kupumzika nk.Hizo zote ni tabia ambazo zinaweza kuonyesha jinsi ambavyo hujipendi au huupendi mwili wako.Kama unaupenda utautumia vibaya au kuuharibu?
Love Yourself-Happy New Year 2011

No comments:

Post a Comment